MTOTO WA MIAKA 11 ADAIWA KULAWITIWA KIJIJI CHA MAGANZO KISHAPU MKOANI SHINYANGA - HUHESO DIGITAL BLOG

Breaking

Post Top Ad

Friday 30 August 2024

MTOTO WA MIAKA 11 ADAIWA KULAWITIWA KIJIJI CHA MAGANZO KISHAPU MKOANI SHINYANGA



Na Mapuli Kitina Misalaba


Mtoto wa kiume mwenye umri wa miaka 11 mwanafunzi wa darasa la nne shule ya msingi Jitegemee, mkazi wa kijiji cha Maganzo Wilaya ya Kishapu Mkoani Shinyanga anadaiwa kulawitiwa na kijana mmoja anayekadiliwa kuwa na umri wa miaka 28.


Akizungumza na Misalaba Media Baba wa mtoto huyo, Bw. Idd James, ameeleza kwamba mtoto wake ambaye ni mwanafunzi wa darasa la nne katika Shule ya Msingi Jitegemee, alikuwa akichunga Ng'ombe Jumapili, tarehe 25 Agosti, wakati tukio hilo lilipotokea.


Mtoto huyo alikuwa amekwenda kuchunga kama kawaida, lakini alipokuwa kwenye majukumu hayo, alikutana na kijana mmoja ambaye alidai kuwa mtoto huyo Ng'ombe zake zimekula miti ya nyumbani kwao ambapo mtuhumiwa huyo alimfuata mtoto akamkamata mkono kisha kumlazimisha kumfuata hadi nyumbani kwao.


Kwa mujibu wa maelezo ya mzazi pamoja na mtoto wamesema akiwa nyumbani kwa mtuhumiwa, mtoto alilazimishwa kuvua nguo na hatimaye alifanyiwa kitendo cha ukatili wa kingono baada ya kutishiwa kwa kisu ambapo baada ya tukio hilo, mtoto alirudi nyumbani na kumweleza baba yake kilichotokea.


“ Mtoto wangu anasoma darasa la nne shule ya msingi Jitegemee ana umri wa Miaka 11 huwa kuna utaratibu wa kuchunga Ng’ombe siku ambazo siyo za shule Jumamosi na Jumapili sasa siku ya Jumapili alikuwa anachunga Ngo’ombe badaye kilichotokea katika yale mazingira ambayo alikuwa anachunga akatokea kijana mmoja kwa kumkadilia anaumri wa Miaka 28 ni mtu mzima huwa anapiga debe stendi ya mabasi Maganzo akamwambia wewe mbona umelisha miti ya nyumbani kwetu mtoto wangu akamjibu mbona mimi hata sijafika huko kwenye miti yenu yule kijana anaishi na baba yake akawa amemshika mkono akampelekea hapo kwa baba yake ndo akaenda kumwingiza ndani na kumwamlisha avue akiwa amemtolea kisu kwa vile sasa mtoto ni mdogo akaona bora asalimishe maisha yake akamsikiliza anavyotaka ndiyo akawa amemlawiti”.amesema baba wa mtoto Bwana James


Baba huyo alichukua hatua za haraka kumpeleka mtoto wake kwenye Zahanati ya Maganzo kwa ajili ya vipimo na matibabu ambapo Daktari aliyemhudumia mtoto huyo ni Dkt. Sam Philip.


Bw. Idd James ameeleza kuwa taarifa za tukio hilo aliripoti katika kituo cha polisi cha Maganzo, ambapo polisi walizindua operesheni ya kumsaka mtuhumiwa huyo, ambaye alikimbia mara baada ya tukio hilo.


Mwenyekiti wa Kitongoji cha Bulumbaga, Bw. Nshishi Jagadi, amesema kuwa amepokea taarifa kuhusu tukio hilo na kutoa wito kwa wakazi wa kitongoji hicho kushirikiana na polisi katika juhudi za kumkamata mtuhumiwa.


“Natoa wito kwa wananchi wangu nawaomba kuanzia mimi ngazi mbalimbali na jamii tushirikiane na sungusungu kuweza kulinda kitongoji chetu haya matukio ya namna hii yasijirudie kwa mara ya pili niwaombe wananchi kuwa wanatoa taarifa za matukioa kama haya ili kuweka kinga kwa watu wahalifu kama hawa wasijirudie tena”.


"Tunahitaji kuhakikisha vitendo kama hivi havijirudii tena katika jamii yetu wananchi wote wanapaswa kushirikiana na vyombo vya usalama ili kudhibiti uhalifu wa aina hii."amesema Mwenyekiti Jagadi


Mwenyekiti wa Kijiji cha Maganzo, Bw. Charles Manyenye, ameongeza kuwa wazazi wanapaswa kuchukua tahadhari zaidi wakati watoto wanapokwenda kuchunga, na kwamba ni muhimu kwa watoto kutembea kwa makundi ili kuepuka hatari kama hizi.


“Alinipigia baba mlezi wa yule mtoto akanieleza taarifa kamili ya tukio hilo kitendo hicho kwanza kimenikela sana niwaombe tu wazazi kuwa hawa watoto wanapoenda machungani asiende peke yake wawe wanatembea wawili au watatu kwa sababu vitendo hivi vinataka kukisili sasa, jamii kwa ujumla wachukue tahadhari kwa kweli lakini wazazi wawe wanatoa taarifa mapema inapofikia hatua hiyo”.amesema Bw. Manyenye.


Katibu wa jumuiya ya kupinga ukatili Shujaa wa Maendeleo na Ustawi wa Jamii Tanzania (SMAUJATA) Wilaya ya Kishapu, Ndg. James Onyango Meshack, ametembelea familia ya mtoto huyo na kuwahakikishia wazazi kwamba hatua kali zitachukuliwa dhidi ya mtuhumiwa.


Pia amewasihi wazazi wa mtoto huyo kuwa karibu na kijana wao ili kumsaidia kupunguza msongo wa mawazo na athari za tukio hilo.


Misalaba Media imezungumza na baadhi ya wananchi wakazi wa kijiji cha Maganzo ambao wameliomba hasa jeshi la polisi kufanya jitihada za kumkamata mtuhumiwa ili hatua za kisheria zichukuliwa.


Katika mwendelezo wa juhudi za kupambana na ukatili dhidi ya watoto, jamii ya Maganzo imeombwa kutoa ushirikiano na kuhakikisha kuwa wanatoa taarifa kwa haraka juu ya matukio yanayotishia usalama wa watoto wao.

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Pages

Huheso