MTOTO MWENYE UALBINO AMEKUTWA AMEUAWA, NA VIUNGO VIMEKATWA - HUHESO DIGITAL BLOG

Breaking

Post Top Ad

Monday 17 June 2024

MTOTO MWENYE UALBINO AMEKUTWA AMEUAWA, NA VIUNGO VIMEKATWA






Mtoto Asimwe Novath enzi za uhai wake
Mwili wa mtoto Asimwe Novath ukipakizwa kwenye gari


Na Mariam Kagenda _ Kagera


Mwili wa mtoto mwenye Ualbino Asimwe Novath ambaye alichukuliwa na watu wasiofahamika nyumbani kwao katika kijiji cha Bulamula kata ya Kamachumu wilayani Muleba Mkoani Kagera umekutwa ukiwa umetupwa kwenye karavati na kuondolewa baadhi ya viungo vyake vya mwili katika kijiji cha Marere kata ya Ruhanga wilaya ya Muleba.


Akizungumza leo Juni 17,2024 baada ya kupatikana kwa Mwili huo katibu tawala wilaya ya Muleba Bwana Benjamini Mwikasyege amesema kuwa wamepata taarifa majira ya asubuhi kutoka kwa wasamaria wema walioona mwili huo na baada ya kufika katika eneo hilo walikuta mwili ukiwa umetupwa kwenye Karavati na umekatwa mikono.




Amesema kuwa mwili wa mtoto huyo umepelekwa Mochwari na Jeshi la polisi linaendelea na uchunguzi na baada ya uchunguzi watazungumza na familia ya mtoto kwa ajili ya kumstiri mtoto huyo katika nyumba yake ya milele.


Mtoto huyo aliyekuwa na umri wa miaka 2 na nusu alichukuliwa na watu wasio fahamika nyumbani kwao Mei 30 mwaka huu Majira ya saa moja jioni baada ya watu wawili kuja kuomba msaada wa chumvi kwa mama wa mtoto huyo kisha kumkaba na kuchukua mtoto


Kwa upande wake Afisa mtendaji wa kata ya Ruhanga amesema kuwa alipigiwa simu na mwenyekiti wa kijiji cha Marere kuwa kuna mwili wa mtoto umepatikana katika kijiji hicho ukiwa umetupwa kwenye Karavati hivyo akafanya mawasiliano ngazi ya wilaya na ndugu wa marehemu.


Amesema kuwa katika kata hiyo tukio kama hilo halijawahi kutokea ambapo amewahimiza wananchi kujiepusha na vitendo vya ukatili kwani watu wenye ualbino wanatakiwa kuishi kama ilivyo kwa watu wengine .


Nao baadhi ya wananchi wa kijiji cha Marere kata ya Ruhanga wamelaani kitendo hicho na kuliomba Jeshi la polisi kuwatafuta watu waliohusika na kitendo hicho ili wafikishwe kwenye vyombo vya Sheria .

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Pages

Huheso