MKUU WA KITENGO CHA FEDHA SERENGETI AKAMATWA MADAI YA WIZI WA MILIONI 213 - HUHESO DIGITAL BLOG

Breaking

Post Top Ad

Wednesday 28 February 2024

MKUU WA KITENGO CHA FEDHA SERENGETI AKAMATWA MADAI YA WIZI WA MILIONI 213

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amemwagiza Kamanda wa Polisi mkoa wa Mara, ACP Salum Morcase  amkamate Mkuu wa Kitengo cha Fedha na Uhasibu wa Halmashauri ya Wilaya ya Serengeti, Saad Ishabailu kwa kosa la kuhamisha shilingi milioni 213.74  akishirikiana na watumishi wa  TAMISEMI na kuzitumia kwa matumizi yao binafsi.

 

Ametoa agizo hilo Februari 27, 2024 wakati akizungumza na madiwani na watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Serengeti kwenye kikao kilichofanyika kwenye Halmashauri hiyo, mkoani Mara ambapo Ishabailu anadaiwa kufanya uhamisho kwa awamu nne kwa njia ya uhamisho wa ndani.

 

“Mkamate huyo bwana sasa hivi aende polisi akafunguliwe mashtaka, huyu ni wa kupeleka mahakamani moja kwa moja. DPP aelezwe afungue  jalada la mashtaka. Wale wenzake tumewapeleka mahakamani tayari sababu tulibaini walihusika na wizi kama huu kwenye Manispaa ya Kigoma mwaka jana,   ” ameagiza  Waziri Mkuu.

 

Amesema Juni 21, mwaka  jana Ishabailu alianza kufanya matumizi ya hizo fedha kwa kushirikiana na mfanyabiashara wa Mugumu, Daudi Matinde Chacha kupitia kwenye akaunti zake za NMB na CRDB kwa kupitia miamala minne ya shilingi milioni 76.3, milioni 57.7, milioni 47 na shilingi milioni 32.5.

 

Ameongeza kuwa alipoulizwa na timu ya uchunguzi Matinde alikiri kuwa haidai fedha yoyote Halmashauri ya Serengeti isipokuwa Mweka Hazina huyo aliomba apitishie fedha zake kwenye akaunti zake kwa sababu zinahitajika haraka kwa matumizi ya ofisi.


“Aliambiwa atoe shilingi milioni 189 akamkabidhi zote Ishabailu na zilizobakia (shilingi milioni 24) akaambiwa abaki nazo,” amesema  Waziri Mkuu.

 

Hata hivyo, Waziri Mkuu amewasisitiza madiwani na watumishi kuwa makini na matumizi ya fedha za umma kwani Rais Samia Suluhu Hassan anatafuta fedha na kuzileta kwenye Halmashauri ili zije kutatua kero za wananchi.

 

Chanzo :  Global Publishers

 

No comments:

Post a Comment

Post Top Ad

Pages

Huheso